Na Christina Mbezi,
Dar es Salaam.
Mradi wa Ujenzi na Uwekaji wa Boya Jipya la Mafuta yaliyosafishwa na yasiyosafishwa kwenye Bandari ya Dar es Salaam unatarajiwa kukamilika mwezi Juni kabla ya mradi huo kuanza kutumika rasmi Julai mwaka huu.
Mradi huo utakaogharimu Dola za Marekani Milioni 70 kutoka Mamlaka ya Bandari Tanzania TPA na Benki ya Dunia ukikamilika unatarajiwa kuongeza uwezo wa kupakua mafuta kwenye bandari hiyo kutoka tani za ujazo 40,000 za sasa hadi tani 150,000.
Mradi huo uliotiwa saini Septemba 30 mwaka 2010 baina ya TPA na kampuni ya Leighton Offshore huko Singapore unahusisha utandazaji wa mabomba ndani na nje ya bahari na unatarajiwa kupunguza gharama za usafirishaji wa mafuta kwa kurahisisha upakuaji wake kwenye bandari ya Dar es Salaam, kupunguza msongamano wa meli zinazosubiri kupakua nishati hiyo na kuruhusu uingizaji wa meli kubwa tofauti na ilivyo hivi sasa.
Akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Meneja wa Bandari ya Dar es Salaam Cassian N’gambo amesema hadi sasa ujenzi huo ulioanza Agosti mwaka jana umefikia zaidi ya asilimia Sitini.
Mradi huo utakapoanza rasmi mafuta yasiyosafishwa yanatarajiwa kupakuliwa kwa mita za ujazo wa 3,500 kwa saa na mafuta yaliyosafishwa yatapakuliwa kwa mita za ujazo wa 2,500 kwa saa.
Meli yenye tani 40,000 za nishati hiyo ikitarajiwa kupakuliwa kwa saa 20.
Mwisho










